KANUNI za ligi zingebadilishwa tangu msimu uliopita kuwa timu zikifanana idadi ya pointi mwisho mwa ligi basi ile ambayo ilipata alama nyingi zaidi mwenzake  walipokutana basi Simba ndiyo ingekuwa bingwa wa ligi badala ya Yanga.

Simba na Yanga zilimaliza ligi msimu uliopita zikiwa sawa pointi 68 kila mmoja lakini Yanga walitwaa ubingwa kutokana na kuwa na tofauti kubwa zaidi ya mabao ya kufunga na kufungwa.

Rais wa Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi alisema kuanzia msimu ujao endapo timu mbili zitamaliza ligi zikiwa na pointi sawa basi wataangalia nani alimfunga mwenzake (head to head) kama suala hilo litapitishwa na Kamati ya Utendaji.

Kikosi cha Simba na viongozi wao ambao wangeweza kuwa mabingwa kama tu kanuni hii ingetumika tangu mwanzoni mwa msimu

“Kamati ya utendaji itakaa na kuangalia kuanzia msimu ujao kanuni za ligi zibadilishwe na endapo timu mbili zitafungana alama basi bingwa ataamuliwa kwa matokeo ya head to head,” alisema Malinzi.

Malinzi alisema kuwa mfumo huo umekuwa ukitumiwa sana sehemu mbalimbali duniani ambapo hata timu ya Taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17 ‘Serengeti Boys’ ilitolewa kwa kanuni hiyo katika fainali za vijana zilizofanyika Gabon mwezi uliopita.

“Ukiangalia vijana wetu wa Serengeti walimaliza wakiwa na pointi nne sawa na Niger lakini wenzetu walisonga mbele kwakua tulivyokutana walitufunga kwahiyo hata sisi tumeona sio mbaya kutumia kanuni hizo,” alisema Malinzi.

Msimu uliopita Simba iliifunga Yanga katika mchezo wa pili baada ya sare kwenye mchezo wa kwanza hivyo kanuni hizo zingekuwa zinatumika basi Simba angekuwa bingwa kwa msimu wa 2016/17.

Post a Comment

 
Top