YAMESALIA masaa matano tu Wekundu wa Msimbazi Simba waingie dimbani kupambana na Mbao FC kwenye mchezo wa fainali ya kombe la Shirikisho (ASFC) huku vijana hao wa Rais Evans Aveva wakiingia uwanjani na ‘ushindi’ wa 2-0 vichwani mwao.

Makocha, wachezaji na hata mashabiki kwa nyakati tofauti wamekiri ugumu wa mechi hiyo kutokana na mambo kadhaa yakiwemo matokeo ya timu hizo katika michezo yao ya hivi karibuni.

Simba wameukosa ubingwa wa ligi kuu ya Vodacom ambao umeelekea kwa watoto wa Jangwani Yanga hivyo nafasi yao pekee kushiriki michuano ya kimataifa ni kwa kutwaa ubingwa leo hii ambao unatolewa macho na Mbao.

Mbao imekuwa ikivisumbua vigogo Simba na Yanga ambapo katika mechi tatu ilizokutana na Yanga imeshinda mbili jijini Mwanza na kupoteza moja ambayo ilichezwa jijini Dar es Salaam hivyo unaweza kusema “Mbao 2-1 Yanga.”

Kwa upande wa Simba wao licha ya kupewa wakati mgumu sana inapokutana na Mbao, wamefanikiwa kuibuka na ushindi katika mechi zote mbili walizokutana huku Mbao wakishindwa kuambulia chochote na kauli rahisi ni kusema “Simba 2-0 Mbao.”

Kwa mantiki hiyo Simba inaingia uwanjani alasiri ya leo ikiwa na historia nzuri dhidi ya Mbao ambao wanapambana kuweka historia mpya kushiriki michuano ya kimataifa katika msimu wa kwanza tu tangu kupanda daraja na kushiriki ligi kuu.

Post a Comment

 
Top