NASIKIA hainaga ushemeji tunakulaaa, nasikia hainaga ushemeji tunakulaga, nasikia haina ushemeji tunakula, nasikia hainaga ushemeji tunakulaga. Wanangu zamu ya nani leo? Zamu ya Man Fongo, zamu yako itakuja kesho usijali baharia wangu.
Hayo ni baadhi ya mashairi yaliyomo kwenye wimbo wa Aman Hamisi ‘Man Fongo’ uitwao Hainaga Ushemeji, wimbo huo umefanya vizuri na kusababisha mashabiki mbalimbali kuupenda muziki wa singeli.
Muziki huo wa singeli ambao umejikusanyia mashabiki wengi, unatokana na midundo yake na staili wanayoimba.
Mbali na kibao hicho cha Hainaga Ushemeji, kuna singo nyingine kali kama Kazi Kazi ulioimbwa na Mbunge wa Jimbo la Mikumi kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Joseph Haule ‘Profesa Jay’, akimshirikisha Sholo Mwamba.
Nyingine ni Nioe Kabila Gani wa MC Sudi, Matobo ya Msaga Sumu na Elena ya chipukizi wa muziki huo, Moto Kombati.
Muziki huo wa singeli unaonekana kupita njia kama zile zilizopita muziki wa hip hop, ambao baadaye ukasababisha kuibuka kwa muziki wa Bongo Fleva.
Mwanzoni mwa muziki huo wa singeli ulionekana kama ni uhuni, kama vile ilivyokuwa ule wa hip hop, zama za akina Saleh Jabir, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ (Mbunge wa Chadema Mbeya Mjini), Balozi Dola Soul na makundi mbalimbali ya muziki zama hizo.
Kipindi hicho walikuwa wanashiriki matamasha bila hata kulipwa, lakini mwisho wa siku walipenya taratibu mpaka kuweza kueleweka katika jamii kwa kufanya kazi nzuri wala si uhuni tena.
Hili limejidhihirisha katika matamasha mbalimbali, likiwemo lile la Fiesta Imooo mwaka huu, ambapo wakali wa singeli, Man Fongo na Shola Mwamba walitamba sana na kuwapagawisha mashabiki wao.
Wakali hao waliteka hadhira kwa jinsi walivyokuwa wakiimba na kucheza na kuwafanya mashabiki hao kuwashangilia sana.
Lakini haikuwa rahisi kwa muziki huo wa singeli kuweza kupata nafasi ya kusikika, kwa kuwa wengi waliuchukulia kama uhuni, kutokana na muziki huo kufanywa mitaani na usiku ambapo kila unapofanyika huzuka fujo na mara nyingine unyang’anyi.
Juhudi za waimbaji wa singeli kwa kiasi kikubwa zimesababisha muziki huo kupenya kwa nguvu.
Mwanzoni muziki huo ulianza kuchezwa katika vituo vya redio, runinga japo kwa muda mfupi, kwani ilikuwa ikihofiwa jamii wanaweza wasiwaelewe, lakini sasa umepokelewa na kuonekana kukaribia kuupoteza muziki wa Bongo Fleva.
Kwa sasa kila ukisikiliza nyimbo za singeli unaweza kuona kabisa zama za Bongo Fleva zimeanza kupitwa na wakati, kwa jinsi wasanii wa singeli wanavyokubaliwa kila sehemu.
Sasa nyimbo kama Hainaga Ushemeji, Kazi Kazi, Nioe Kabila Gani inasikilizwa na watu wa rika zote kutokana na ujumbe uliomo kwenye nyimbo hizo.
Ni wazi muziki huo wa singeli utaendelea kufanya vizuri na kuzidi kuipoteza Bongo Fleva na bila shaka sasa hii itakuwa zamu ya wasanii wa singeli kutesa ndani na nje ya mipaka ya Tanzania, kwani mashabiki wa Bongo Fleva wameonekana kupokea kwa kasi muziki huo wa singeli kwa nguvu na hata wakipanda jukwaani wasanii hao wamekuwa wakipokelewa kwa shangwe kubwa na kuwafunika wakali wa Bongo

Post a Comment

 
Top