WINGA wa Azam FC, Ramadhan Singano, ameuweka mtegoni uongozi wa klabu hiyo baada ya kukwepa kusaini mkataba mpya.
Nyota huyo, aliyejiunga na Azam akitokea Simba, amemaliza kandarasi ya miaka miwili ya klabu hiyo iliyo na maskani yake Chamazi, jijini Dar es Salaam.
Meneja wa Azam FC, Philipo Alando, alisema hatima ya mchezaji huyo klabuni kwao haijulikani, kutokana na kutoanika kama ataongeza mkataba au la.
“Tumeshakutana na Singano na kuzungumza naye juu ya mkataba mpya, lakini bado hajatoa jibu kama ataendelea na timu yetu au la na sisi tumemuacha achague.
“Kwa sasa hatumlazimishi mtu kusajili, ndiyo maana tunatoa nafasi kwao ya kuchagua kama wanahitaji kuwa nasi au la, hata Singano bado ana nafasi ya kuangalia wapi anaona ni sahihi kwake kufanya kazi,” alisema.
Azam tayari imeachana na wachezaji wake watatu waliotimkia Simba, ambao ni straika John Bocco, kipa Aishi Manula na Shomari Kapombe.
Post a Comment