Baada ya Msimu wa ligi kuu Tanzania bara mwaka 2016/2017 kumalizika huku Klabu ya Yanga ikinyakua taji hilo kwa mara ya tatu mfululizo , sasa ni wakati wa kujiandaa na msimu mpya wa ligi kuu unaotegemewa kuanza kutimua vumbi Mwezi September mwaka huu .
Wakati tukisubiri hadi msimu mpya kuanza , si vibaya tukazijua vizuri timu tatu zilizofanikiwa kupanda ligi kuu msimu wa 2017/2018.
Singida United
Hii ni timu ambayo inapewa nafasi ya kuweka Historia kwa kupanda ligi kuu na kuchukua ubingwa wa ligi kuu .
Singida United inapanda ligi kuu baada ya kukaa miaka 17 bila kuionja ligi hiyo . Kuna kila sababu ya timu hii kusumbua katika msimu mpya wa ligi kuu .
Sababu ya kwanza ni usajili wa aliyekua mkurugenzi wa ufundi na kocha wa zamani wa Yanga, Mholanzi , Hans Pluijm . Akiwa Yanga , Pluijm aliweza kuisaidia timu hiyo kuwa bingwa wa ligi kuu Tanzania bara mara mbili mfululizo tangu msimu wa 2014/15 na 2015/16 pamoja na kushiriki hatua ya robo fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.
Kingine kitakachoifanya Singida United itambe msimu ujao ni udhamini wa shilingi milioni 250 kwa mwaka kwa kipindi cha miaka mitano walioupata kutoka kwa Kampuni ya Michezo ya Kubashiri ya Sportpesa. Mkataba huu pia utaipa Singida United bonus nyingine kama watachukua ubingwa wa Ligi Kuu Bara au Kombe la Kagame au ubingwa wa Afrika.
Lipuli FC
Lipuli FC ya Mkoa wa Iringa ndiyo iliyokuwa timu ya kwanza kupanda Ligi Kuu Bara kwa msimu ujao wa 2017-2018 baada ya kushika nafasi ya kwanza kwenye kundi A la ligi daraja la kwanza.
Lipuli FC inarejea kwenye ligi kuu Tanzania bara baada ya kupita zaidi ya miaka 13 tangu iliposhuka daraja miaka ya mwanzoni mwa 2000.
Lipuli FC inaingia kwenye ligi kuu Tanzania bara ikiwa na changamoto ya kiuongozi baada ya viongozi wake kuingia kwenye mgogoro wa kiongozi hali iliyofanya Chama cha mpira mkoani Iringa (IRFA) kuichukua timu na kuunda kamati ya kuisimamia .
Njombe Mji
Njombe Mji inapanda Ligi Kuu kutoka kundi B baada ya kuifunga Mafinga goli 2 – 0 na kufikisha pointi 22 ambazo wapinzani wake , klabu za KMC, Polisi Morogoro na JKT Mlale wasingeweza kuzifikia .
Kikubwa tunachojua kuhusu timu hii ni taarifa iliyotolewa kuwa wamepata maombi ya wachezaji 80 walioachwa na timu zilizokua zinashiriki ligi kuu bara na nje ya nchi huku wakithibitisha tayari kuanza kuwafanyia majaribio baadhi ya wachezaji hao .
Tayari uongozi wa chama cha soka mkoani Njombe (NJOREFA) umeahidi kukarabati uwanja wa Sabasaba ili kuruhusu mechi za ligi kuu zipigwe kwenye uwanja huo .
Post a Comment