MAKAMU wa Rais wa Simba, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’, amerejea nchini juzi akitokea Zimbabwe, huku akionekana kuichezea akili Yanga ambayo tayari imetamba kutokuwa tayari kuwaona watani wao hao wa jadi wakiwapora ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Japo Simba ipo kileleni mwa ligi hiyo ikiwa na pointi mbili zaidi ya Yanga, iliyojikusanyia pointi 33 baada ya kila timu kushuka dimbani mara 15, bado Wanajangwani hao wameonekana kutotishika hata kidogo.
Kitendo hicho, yaani jeuri ya Yanga, kimekuwa kikiwashangaza watu wa Simba, hali inayowafanya wajiulize mara mbili mbili.
Kati ya majibu waliyoyapata watu wa Simba juu ya tambo za watani wao hao, ni ubora wa kikosi cha Yanga, hasa katika suala zima la makali ya safu ya ushambuliaji, inayoundwa na Mzimbabwe Donald Ngoma, Mrundi Amis Tambwe na winga hatari, Simon Msuva.
Baada ya kubaini hilo, Simba iliamua kutupia macho kwingineko kuona kama inaweza kukiboresha zaidi kikosi chake kupitia dirisha dogo la usajili, ambalo limeshafunguliwa tangu Jumanne, wiki hii.
Hapo ndipo ilipoamua kufunga safari hadi Zimbabwe kuona kama inaweza kupata mshambuliaji wa kiwango cha juu zaidi ya Ngoma, ili kusaidiana na wakali waliopo Msimbazi kama Ibrahim Ajib, Shiza Kichuya na Mrundi Laudit Mavugo.
Japo viongozi wa Simba wamekuwa wakishindwa kuweka wazi juu ya hilo, lakini hakuna shabiki yeyote wa soka hapa nchini asiyefahamu kuwa, Kaburu alikuwa Zimbabwe tangu mwishoni mwa wiki iliyopita.
Kaburu aliondoka nchini akiwa pamoja na msafara wa timu ya Taifa, Taifa Stars, akiwa kama kiongozi wa msafara, lakini cha kushangaza japo timu hiyo ilirejea tangu Jumatatu, Kaburu aliendelea kubaki nchini humo kama alivyokiri jana alipozungumza na BINGWA.
Kitendo cha Kaburu kukaa Zimbabwe kwa takribani siku tatu baada ya mechi ya Stars, kimeonekana kuwashtua mashabiki wa Yanga, wakiamini lazima kuna kitu amekifanya huko, zaidi ikiwa ni suala zima la kufanya mazungumzo na mchezaji kama si wachezaji.
Kwa bahati nzuri, Zimbabwe kuna mchezaji wa Simba, Justice Majabvi, ambaye ndiye aliyewawezesha Wekundu wa Msimbazi hao kumnasa beki hodari, Method Mwanjali.
Alipoulizwa iwapo alipokuwa Zimbabwe kuna habari njema zozote anazoweza kuwapa watu wa Simba, kuhusiana na suala zima la usajili, Kaburu alisema: “Suala la usajili lipo mikononi mwa kocha, benchi la ufundi ndilo linalofahamu ni mchezaji gani wa kusajiliwa na si kiongozi.
“Mimi nilikwenda Zimbabwe nikiwa kama mkuu wa msafara wa timu ya taifa na baada ya mechi nilibaki huko kwa ajili ya shughuli zangu za kazi, ndio nimerudi jana (juzi).”
Kaburu alikuwa akitoa kauli hiyo huku akionekana kuwa na furaha mno, hali inayoashiria lazima kuna jambo litatokea hivi karibuni, ukizingatia kiongozi huyo amekuwa akifahamika zaidi kutokana na umafia wake wa kufanya kila awezalo kufanikisha jambo lolote analolitaka au analoagizwa na klabu yake hiyo.
Kinachoonekana, Kaburu anawazuga watani wao, Yanga, kutokana na kile ambacho Wekundu wa Msimbazi hao wamekuwa wakikieleza, kutotaka kuweka mambo yao wazi kwa kuhofia figisu figisu za wapinzani wao.
Simba wanaonekana kuendelea kukumbuka jinsi Yanga ilivyowaliza kwa Mbuyu Twite, ambapo baada ya kuamini kuwa kiungo huyo ni mali ya Msimbazi, watani wao hao kupitia kwa aliyekuwa Mjumbe wa Kamati ya Usajili, Abdallah Bin Kleb, waliwazidi ujanja na hatimaye nyota huyo aliyekuwa akikipiga APR ya Rwanda kwa mkopo akiwa ni mali ya DC Motema Pembe ya DRC Kongo, alitua Jangwani.
Mbali ya Twite, pia Yanga iliwazidi ujanja Simba kwa aliyekuwa beki wao, Kelvin Yondani, mshambuliaji Emmanuel Okwi, Juma Mahadhi na wengineo.
Dirisha dogo la usajili linatarajiwa kufungwa Desemba 15, mwaka huu, ambapo kwa sasa timu shiriki zinahaha kuviimarisha zaidi vikosi vyao tayari kwa mzunguko wa pili wa ligi hiyo yenye timu 16.
Post a Comment